Wednesday, September 27, 2017

MAKALA; Aslay na kuvunjika Yamoto Band



Na Mohamed Mussa
 TANGU siku ya kwanza ilipotangazwa kuvunjika kwa bendi ya Yamoto, mwanamuziki kiongozi wa bendi hiyo Aslay Isihaka amekuwa akiachia nyimbo na video mpya kila kukicha na kuzua maswali mengi.


Mashabiki wa bendi hiyo na mwanamuziki Aslay wengi wamekuwa wakijiuliza na kufikiria kwamba mwanamuziki huyo huenda alijiandaa kuachana na bendi hiyo ndio maana aliamua kuandaa nyimbo nyingi ambazo zinaingia sokoni sasa.
Aslay anasema hadi sasa tangu walipoachana na bendi hiyo Machi 2017, walipotembelea nchi saba za Ulaya tayari ameshatoa nyimbo 12 na bado anatamani kutoa nyingi zaidi.
Kwa sasa Aslay anafanya kazi na meneja  Yusufu Chambuzo ambaye ni mwaasisi wa kituo cha  Mkubwa na Wanawe pia ni mwalimu na mwazilishi wa Yamoto Band.
Akizungumza na mwandishi wa  makala hii, Chambuso alianza kufafanua  kwa kusema yeye, Amani Temba na Saidi Fella ndio walioanzisha kituo cha Mkubwa na Wanawe mwaka 2012 .
Kwa mara ya kwanza kituo hicho anasema kiliundwa na watu wanne akiwemo na Suresh maarufu kama Mr India anayemiliki studio ya Eyooo ambaye alitengeneza kazi za Bibi Cheka na  Dogo Aslay nanda kusema kwa mama.
Anasema kutokana na kukosa maelewano na Suresh alijitoa na kituo hicho kuendelea na kazi zake mpaka ilipokuja kuibuka makundi mengi ikiwemo Yamoto.



Anasema kufikia machi  2017 baada ya kurudi kutoka kufanya matamasha katika nchi saaba za Ulaya, wasanii walianza kulalamika kwamba wanahitaji kufanya kazi kujipima uwezo wao.
Anasema kikubwa kwamba kila msanii alihisi kipato alichokuwa akikipata kilikuwa hakimtoshi, hivyo alihitaji nafasi ya kufanya kazi zaidi.
“Ilinichanganya sana kwakuwa mimi nilitumia muda mwingi wa maisha yangu katika kuandaa wasanii kama Yamoto, lakini leo wanataka kugawanyika huku nikiwa sijapata chochote,” alisema.
Chambuso anasema yeye ndio mtu ambaye alikuwa akiwafundisha wanamuziki wa Yamoto, kwakuwa alikuwa na ujuzi na  alishapitia  bendi mbalimbali za muziki  hadi bendi za muziki wa asili.
“Mimi nimeimba sana katika bendi, hivyo ninaweza kupiga ngoma, gitaa, kinanda tumba na vifaa vingine huku nikiwa na uelewa mkubwa wa muziki,” alisema.
Anasema ujuzi huo aliamua kuutumia kwaajili ya kuwafundisha Yamoto, kwakuwa  aliamini mafanikio ya  bendi hiyo kungeweza kumletea manufaa katika maisha yake badala yake ikawa tofauti.
“Kwakuwa wasanii walitaka kutengana kila mtu kufanya kazi yake uongozi  tulikaa chini, tukapitisha wacha wafanye ili wawe huru,” anasema.
Anasema baada ya Yamoto kutawanyika kwaajili ya kutafuta maslahi nje ya kundi, aliamua kuachana na muziki na kuamua kufanya kazi zingine.
Anasema kwa muda wa miaka yote hiyo hakuna ambacho anakimiliki, kutokana na muziki ingawa alikuwa kiongozi wa juu mwanzilishi na na mwalimu.
Anasema yote hayo yalitokana na uongozi mbaya waliokuwa nao ingawa muziki ulikuwa ukiingiza fedha nyingi.
Chambuso anasema hataki kusema kwamba anamlaumu Saidi Fella, kwakuwa ndio mtu aliyemfundisha njia za uongozi ingawa anatamani kuja kuwa kiongozi mzuri.
Anasema ingawa bendi hiyo ilikuwa ikifanya vizuri  wanamuziki  hawakuwa na chochote cha kujivunia, ndio maana wakatamani kufanya maisha ya kujitegemea.
Baada ya kutoa wimbo wa mwisho wa Basi,  kila mmoja alianza kuhangaika kivyake ili aweze kuongeza Kipato, ndipo Aslay alipoachia nyimbo kama , Kidawa, Angemuona na Tete ambapo zilianza kufanya vizuri.
“Baada ya kutoa nyimbo hizo alinifuata na kuniambia kwamba ananihitaji kwaajili ya kufanya kazi ya pamoja,” anasema.
Anasema aliamua kuungana naye ambapo walifungua ofisi, lakini muda huo huo mtayarishaji wa muziki wa Yamoto Shirko naye aliwafuata na kutaka wafanye kazi pamoja.
Wanamuziki wengine akiwemo mwanamuziki wa Zanzibar Berry Black, Osama, Podo, Kingo Master na K Young wote walikuwa Mkubwa na Wanawe waliahama kumfuata.
“Nilipoona wanakuja wengi niliwasimamisha na kuwaambia hata hii ni sawa na Mkubwa na wanawe kwakuwa uongozi ni ule ule ,” alisema.
Alisema muda mchache wakafungua ofisi na kupata vifaa na tayari wakaanza kufanya kazi kwa wingi.
Meneja Chambuso amesema bado yupo katika kituo cha Mkubwa na Wanawe, kwakuwa haki zote za umiliki bado zipo pia anatoa msaada wa ushauri kwa wasanii wa kituo hapo.
Lakini mwisho pia alisema nyumba ambazo wanamuziki wa Yamoto walizopewa ni za kwao kweli, isipokuwa kukamilisha kupewa nyumba hizo ndio bado hadi leo.
Pia mwanamuziki Aslay Isihaka ambaye kwa sasa anajiita Dingi Mtoto, alifafanua zaidi anasema aliamua kufanya kazi na meneja Chambuso kwakuwa ndio mtu anayeujua mziki wake.
“Baada ya kila mwanamuziki kutaka kufanya kazi kivyake niliona bora nifanye kazi na Chambuso kama meneja wangu, sababu yeye ndiye aliyenipokea na kunifundisha muziki,” alisema.
Anasema kwa sasa hana ugonvi na mwanamuziki mwezake wa Yamoto kwakuwa hawakuachana kwa ugonvi na kilichopelekea kutengana kwa muda ni kutokana na maslahi ya kazi zao.
Alisema hivi sasa wanastudio na ofisi Mwembe Yanga Temeke, ambapo mara ya kwanza alitamani kitu hicho kiwe Sinza lakini ilishindikana.
“Nilipata nyumba Sinza wakanikubalia lakini nilipowaambia anataka kufungua studio ya Muziki walikataa, ikabidi ofisi tuhamishie Temeke Mwembe Yanga,” alisema.
Alizitaja nyimbo ambazo alizitoa baada ya kutoka Mkubwa na Wanawe kuwa ni Kidawa, Tete, Rudi, Mario, Angekuona, Autegeki, Ndoa, Likizo, Baby, Danga, Pusha na Mhudumu.
Alisema hadi sasa ananyimbo zaidi ya 32, ambazo bado hajazitoa na yupo katika mikakati ya kuzitoa.
“Malengo yangu nikuufikisha muziki wangu mbali zaidi, najiona nimekuwa mpya kwakuwa najiamini kwa sasa,” alisema.
Anasema tayari ameshaanza kutambulika zaidi kwa kazi zake na tayari amekuwa akipata matamasha mengi mkoani na Dar es Salaam.
Alisema kwa sasa amekuwa na mendeleo kidogo kwakuwa aliondoka kwaajili ya kutafuta maendeleo, ambayo kwa sasa anayaona japo kidogo.
Wakati huo huo Meneja Chambuso amesema kwa sasa amefanikiwa kunua gari dogo kwa muda wote wa maiasha yake ya kimuziki, jambo ambalo anahisi anaanza kupata nafuu kwa kile ambacho alikuwa akikifanya kwa miaka yote.
Mwisho
 By Mohamed M Gomesa (Habari Leo) 0714956288

No comments:

Post a Comment

https://www.facebook.com/gomesamohamedi